Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

NATIONAL PROSECUTIONS SERVICES

NAIBU KATIBU MKUU AFUNGUA JENGO JIPYA LA OFISI YA TAIFA YA MASHTAKA MKOANI SHINYANGA
16 Mar, 2024
NAIBU KATIBU MKUU AFUNGUA JENGO JIPYA LA OFISI YA TAIFA YA MASHTAKA  MKOANI SHINYANGA

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria Dkt. Khatibu Kazungu leo tarehe 16 Machi, 2024 amefungua jengo jipya la Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoani Shinyanga lililopo katika eneo la Uzunguni.

Akizungumza katika ufunguzi huo Naibu Katibu Mkuu amewataka watumishi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka kuimairisha na kuboresha utendaji kazi kutokana na Serikali kuboresha mazingira ya kufanyia kazi kwa kujenga majengo ya kisasa ili waweze kutoa huduma bora za kimashtaka kwa wananchi.

 Pia Naibu Katibu Mkuu amefungua jengo jipya la  Ofisi  ya Taifa ya  Mashtaka  Mkoa wa Shinyanga kwa niaba ya Mikoa mitano ambayo majengo yake yamekamilika ikiwemo Mkoa wa Pwani, Ilala, Manyara, Katavi na Rukwa.

Mkurugenzi wa Mashtaka nchini Slyvester Mwakitalu amesema kukamilika kwa mradi huo wa ujenzi wa jengo jipya la Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoani Shinyanga na maeneo  mengine itasaidia kuboresha na kuimarisha utendaji wa shughuli za uendeshaji wa mashtaka

Mwakitalu amesema mpaka sasa wamekwisha fungua Ofisi za Kimashtaka katika Wilaya 92 za Tanzania bara hali inayochangia kusogeza karibu huduma kwa  wananchi na kuwaondolewa usumbufu wa kusaifiri umbali mrefu.

Aidha Mwakitalu amesema mradi wa Shinyanga umegharimu bilioni 2.153 hadi kukamilika kwake ikijumuisha thamani za ndani ya ofisi hiyo pamoja na miundo mbinu yote.

Kwa upande wao baaadhi ya viongozi waliohudhuria hafla hiyo akiwemo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Shinyanga Mhe. Frank Maimbali amewataka Watumishi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka kuongeza kasi na ufanisi katika uendeshaji wa mashataka kwa kuwa mazingira ya kazi yameboreshwa na kuimarishwa.

Naye Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya  Utawala, Katiba na Sheria Mhe. Boniface Butondo amepongeza kwa hatua zilizopigwa za kuimairisha ofisi za mashataka katika mikoa mbalimbali hivyo matarajio ya kamati ni kuona mashauri mengi yana kwenda kwa kasi kubwa.

Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai nchini DCP Stella Butabihilwa amesema kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kuimairisha ushirikiano wake na Ofisi ya Taifa ya Mashataka kwa kuwa wamekuwa wakishirikiana  kwa hali na mali.

Kwa upande wake mwakilishi wa Kamishna Jenerali wa Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA)  ambaye ni Kamishna wa Huduma za Sheria wa mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Bi.  Veronica Matikila amesema jitihada kubwa zinafanywa na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka katika kusogeza huduma karibu na wananchi 

Bi. Veronica amesema uwepo wa ofisi hiyo ni tija kwao kwa kuwa wamekuwa wakitumia  katika shughuli zao na kuwaletea tija kubwa.